Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt.
Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) (katikati), Waziri wa Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi (kulia) na Rais wa Shirikisho
la Mpira wa Miguu Tanzania- TFF, Bw. Wallace Karia (kushoto) wakiwa
katika picha ya pamoja baada ya kukutana na kufanya majadiliano kuhusu
maendeleo na changamoto zinazoikabili sekta ya michezo hususan mpira wa
miguu nchini, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar es
Salaam.
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt.
Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) (katikati), na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi (watano kulia) wakiwa katika
picha ya pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-Maamry
Mwamba, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha (wa nne kushoto), Naibu
Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bw. Elijah Mwandumbya (wa nne kulia),
Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania, Bw.Yusuph Mwenda (wa tatu kulia)
na viongozi waandamizi wa Wizara ya Fedha, pamoja na Taasisi
zinazosimamia michezo nchini, baada ya kukutana na kufanya majadiliano
kuhusu maendeleo na changamoto zinazoikabili sekta ya michezo hususan
mpira wa miguu nchini, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar
es Salaam.
Raisi wa TFF Wallace Karia pamoja na viongozi wa Bodi ya ligi wakifuatilia jambo wakati wa majadiliano ya maendeleo ya sekta ya michezo na viongozi wa serikali.
Raisi wa TFF Wallace Karia akizungumza jambo wakati wa majadiliano ya maendeleo ya sekta ya michezo na viongozi wa serikali
Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), alikutana na Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Profesa Palamagamba Kabudi, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, Jijini Dar es Salaam, kwa ajili ya majadiliano kuhusu maendeleo na changamoto zinazokumba sekta ya michezo, hasa mpira wa miguu nchini.
Katika majadiliano hayo, Serikali ilitoa pongezi kwa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Bodi ya Ligi kwa usimamizi mzuri wa maendeleo ya soka, ikiwa ni pamoja na heshima kubwa iliyoletwa kwa Taifa kwenye bara la Afrika. Serikali ilitambua juhudi za TFF katika kuandaa mashindano ya CHAN na AFCON, na pia ikakubaliana kuhusu namna tasinia ya utamaduni, sanaa, na michezo inavyoweza kutumika kuhamasisha uzalendo wa kulipa kodi kwa hiari, kupitia kampeni ya kudai na kutoa risiti kwa ajili ya maendeleo ya nchi.
Rais wa TFF, Bw. Wallace Karia, alikubaliana na mapendekezo ya Serikali na alisisitiza kuwa ulipaji kodi ni jambo muhimu kwa maendeleo ya Taifa. Aliahidi kuwa TFF itachukua hatua madhubuti kuhakikisha suala hili linazingatiwa kwa umakini katika michezo yote ya mpira wa miguu inayoendeshwa na Taasisi hiyo.
Majadiliano hayo pia yaliwashirikisha viongozi wa Wizara ya Fedha, akiwemo Katibu Mkuu, Dkt. Natu El-Maamry Mwamba, Naibu Katibu Mkuu, Bw. Elijah Mwandumbya, Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Yusuph Mwenda, Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi, Bw. Almas Kasongo, na viongozi wengine waandamizi wa Wizara ya Fedha na Taasisi zinazohusika na michezo nchini.