Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt.
Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), akizungumza wakati akifungua Mkutano wa
Majadiliano ya Ngazi ya Juu kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo,
uliofanyika katika ukumbi wa Kambarage-Treasury Square, jijini Dodoma,
ukiwahusisha baadhi ya Mawaziri wa Kisekta kutoka Tanzania Bara na
Tanzania Visiwani, pamoja na Wanadiplomasia na Washirika wa maendeleo
wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini.
Mwenyekiti Mwenza wa Kundi la
Washirika wa Maendeleo na Balozi wa Ireland nchini, Mhe. Nicola Brennan,
akizungumza wakati wa Mkutano wa Majadiliano ya Ngazi ya Juu kati ya
Serikali na Washirika wa Maendeleo, uliofanyika katika ukumbi wa
Mikutano wa Kambarage-Treasury Square, jijini Dodoma, ukiwahusisha
baadhi ya Mawaziri wa Kisekta kutoka Tanzania Bara na Tanzania Visiwani,
pamoja na Wanadiplomasia na Washirika wa maendeleo wanaoziwakilisha
nchi zao hapa nchini.
Baadhi ya Washirika wa
Maendeleo nchini wakifuatilia hotuba ya Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt.
Mwigulu Lameck Nchemba (Mb) (hayupo pichani), wakati wa Mkutano wa
Majadiliano ya Ngazi ya Juu kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo,
uliofanyika katika ukumbi Mikutano wa Treasury Square, jijini Dodoma,
uliowahusisha baadhi ya Mawaziri wa Kisekta kutoka Tanzania Bara na
Tanzania Visiwani, pamoja na Wanadiplomasia na Washirika wa maendeleo
wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini.
Na. Farida Ramadhani na Joseph Mahumi, Dodoma
Waziri wa Fedha, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba (Mb), amesema kuwa Serikali inaendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na ukuaji wa uchumi nchini.
Dkt.
Nchemba aliyasema hayo jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano wa
Majadiliano ya Kimkakati kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo
Ngazi ya Juu, ambao unalenga kubadilishana maarifa, taarifa, na uzoefu
kuhusu sera na mikakati ya maendeleo ya nchi.
Alisema
Serikali imewasilisha bungeni Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania
(Tanzania Investment Act, 2024) na kuanzisha Mamlaka ya Uwekezaji na
Maeneo Maalum ya Kiuchumi (Tanzania Investment and Special Economic
Zones Authority) ili kuboresha mazingira ya uwekezaji.
“Serikali
kupitia Chemba ya Biashara, Viwanda na Kilimo Tanzania (TCCIA) na Kituo
cha Uwekezaji kati ya Sekta Binafsi na Umma (CPPP) imeendeleza
majadiliano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi ili kuongeza ushiriki
wa sekta binafsi katika maamuzi”, aliongeza Mhe. Dkt. Nchemba.
Mhe.
Dkt. Nchemba ambaye ni Mwenyekiti wa Mkutano huo, alisema Serikali pia
inaandaa Mkakati wa Kitaifa wa Uendelezaji wa Uwekezaji (2025/2026 –
2034/2035) ambao utakuwa na mpango wa utekelezaji, ufuatiliaji na
tathmini, unaoeleza majukumu ya kila mdau na viashiria vya kupima
maendeleo.
Dkt.
Nchemba alibanisha kuwa katika kipindi cha mwezi Julai 2024 hadi
Desemba 2024, Serikali imeongeza uwezo wa uzalishaji umeme kwa asilimia
30.3, hasa kupitia Mradi wa Umeme wa Maji wa Julius Nyerere (JNHPP) ili
kupunguza gharama za biashara.
“Kupitia
Sheria ya Fedha ya mwaka 2024, Serikali imepunguza au kuondoa ada na
tozo mbalimbali ili kuboresha mazingira ya biashara”, aliongeza Mhe.
Nchemba.
Dkt.
Nchemba alisema Serikali pia imepata mafaniko makubwa katika ukuaji wa
uchumi jumuishi ambapo idadi ya shule na wanafunzi imeongezeka, vituo
vya afya vimeongezeka na huduma zimeboreshwa, huduma za maji
zimeongezeka katika maeneo yote nchini pamoja na ongezeko la ajira.
Aidha,
alitoa rai kwa wadau wote kushirikiana kwa karibu na Serikali ili
kufanikisha utekelezaji wa Mwongozo wa Ushirikiano wa Maendeleo (DCF)
ambao umetilia mkazo utaratibu wa ufadhili wa miradi ya mabadiliko ya
tabianchi (climate financing modality) na kuimarisha Ushirikiano kati ya
Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) kama njia mbadala za ufadhili.
Kwa
upande wake Mwenyekiti Mwenza wa Kundi la Washirika wa Maendeleo na
Balozi wa Ireland nchini, Mhe. Nicola Brennan aliishauri Serikali
kuendelea kuboresha mazingira ya biashara kwa kuondoa vikwazo
vinavyozuia uwekezaji wa moja kwa moja wa kigeni.
Alisema
hii itaongeza mchango wa sekta binafsi katika kuleta uwekezaji, ajira,
uvumbuzi, na suluhisho kwa changamoto mbalimbali ili kujenga uchumi
imara.
“Wadau
wa Maendeleo tayari tumekuwa na majadiliano mazuri kuhusu hili, na
tunapongeza utayari wa Serikali kushirikiana nasi kuona jinsi bora ya
kuondoa vikwazo na kuvutia uwekezaji zaidi wa moja kwa moja wa kigeni
(FDI) nchini Tanzania, pamoja na kuimarisha sekta ya biashara ya ndani”,
aliongeza.
Mhe.
Brennan alisema Washirika wa Maendeleo watahakikisha kuwa Dira ya
Maendeleo ya Mwaka 2050 inapata ufadhili wa uhakika na endelevu, hasa
katika sekta za afya, elimu na sekta ya kijamii kwa ujumla.
“Tunapopanga
vipaumbele katika matumizi ya rasilimali finyu za Msaada wa Maendeleo
(ODA), ni muhimu pia kuelewa vyema vyanzo vingine vya ufadhili
vinavyopatikana kwa nchi zenye kipato cha kati nje ya ODA, pamoja na
mchango ambao sisi kama Wadau wa Maendeleo tunaweza kutoa kusaidia
Tanzania kuzifikia na kuzitumia fursa hizo ipasavyo. Tunatazamia
kujadili zaidi suala hili kwa kina.”
Aliahidi kuwa Washirika hao wataendelea kushirikiana na Tanzania kuhakikisha maendeleo yanapatikana na kustawisha jamii.
Tags
HABARI ZA KITAIFA