FINLAND YAIPONGEZA TANZANIA KWA UTEKELEZAJI WA MIRADI

 
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Christian Omolo, akimkabidhi zawadi Mkurugenzi Msaidizi Idara inayosimamia Afrika, Mashariki ya Kati na Latin America wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Finland, Bi. Helena Airaksinen, baada ya majadiliano ya tathmini ya utekelezaji miradi inayofadhiliwa na nchi hiyo nchini, majadiliano yaliyofanyika, Treasury Square, jijini Dodoma.  
Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Christian Omolo, akizungumza kuhusu miradi inayofadhiliwa na Finland, alipokutana na kufanya mazungumzo na na Mkurugenzi Msaidizi Idara inayosimamia Afrika, Mashariki ya Kati na Latin America wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Finland, Bi. Helena Airaksinen (wa pili kulia), ulioambatana na Balozi wa nchi hiyo Tanzania, Mhe. Theresa Zitting (wa kwanza kulia), walipofika ofisini kwake, Treasury Square, jijini Dodoma.
 
Ujumbe wa Tanzania ukiongozwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Christian Omolo, na Ujumbe wa Finland ukiongozwa na Mkurugenzi Msaidizi Idara inayosimamia Afrika, Mashariki ya Kati na Latin America wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Finland, Bi. Helena Airaksinen wakiwa katika picha ya pamoja baada ya majadiliano ya tathmini ya miradi inayofadhiliwa na Finland, yaliyofanyika jijini Dodoma.

 
Na. Peter Haule, Dodoma

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Bi. Jenifa Christian Omolo, amekutana na kufanya mazungumzo na ujumbe kutoka Finland ukiongozwa na Mkurugenzi Msaidizi wa Idara inayosimamia Afrika, Mashariki ya Kati na Latin America wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Finland, Bi. Helena Airaksinen, ulioambatana na Balozi wa nchi hiyo hapa nchini, Mhe. Theresa Zitting.
 
Akizungumza katika mkutano huo, Bi. Omolo alisema kuwa, ujumbe huo umekuja kwa lengo la kufanya tathmini ya kiutendaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo zilizotekelezwa kupitia msaada wa nchi hiyo kwa kipindi cha mwaka 2021 hadi 2024 ili kupanga mikakati mingine kwa mwaka 2024 hadi 2028.
 
Alisema kuwa tangu mwaka 2010 Finland ilitoa kiasi cha Euro zaidi ya milioni 351 ili kutekeleza miradi mbalimbali ambayo imekamilika kwa takribani asilimia 87 na asilimia 13 ya miradi hiyo bado ipo katika hatua ya utekelezaji.
 
“Makubaliano ya ushirikiano wa kimaendeleo wa hivi karibuni kati ya nchi hizi mbili ulijikita kutekeleza program za maendeleo ikiwa ni pamoja na kuimarisha masuala ya uchumi, kuhamasisha kutengeneza ajira, eneo la ubunifu, kujenga uwezo kuhusu kodi na utawala bora katika kipindi cha mwaka 2021 hadi 2024”, alisema Bi. Omolo.
 
Alisema kuwa kutokana na program kumalizika mwaka 2024 ni dhahiri kunahitajika majadiliano yatakayowezesha kuwa na program mpya zinazotakiwa kutekelezwa kuanzia mwaka 2025.
 
Alisema katika majadiliano hayo Timu za Wataalamu kutoka pande mbili zitaainisha maeneo mapya ya ushirikiano kulingana na Dira ya Taifa ili yaweze kufanyiwa kazi na wadau hao wa maendeleo.
 
Kwa upande wake Mkurugenzi Msaidizi Idara inayosimamia Afrika, Mashariki ya Kati na Latin America wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Finland, Bi. Helena Airaksinen, alisema kuwa maeneo ya ushirikiano kati ya nchi yake na Tanzania yameendelea kuongezeka licha ya kubadilishwa kwa Sera za nchi.
 
Alisema kuwa zipo nchi nyingi ambazo zimeondolewa katika utekelezaji wa program kupitia nchi yake lakini Tanzania itaendelea kuwa mshirika muhimu katika kuchochea maendeleo ya pande hizo mbili kutoka na juhudi zake katika utekelezaji wa miradi mbalimbali.
 
Majadiliano kati ya pande hizo mbili yalihusisha pia wajumbe kutoka Wizara ya Mipango na Uwekezaji, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi maalum, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Madini, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Tume ya Mipango.

Post a Comment

Hii ni Blog kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Nchi yetu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...

Previous Post Next Post