Unknown Unknown Author
Title: MAKALA:: VIJANA KUPEWA MAFUNZO YA UJASIRIAMALI, MAHIZA NAKUPA 'TANO'
Author: Unknown
Rating 5 of 5 Des:
"ukosefu wa ajira kwa vijana ni bomu linalosubiri kulipuka." Kauli hiyo siyo ngeni masikioni mwetu,tumekuwa tunaisikia mara ...
mahiza Mkuu wa mkoa Lindi
"ukosefu wa ajira kwa vijana ni bomu linalosubiri kulipuka."
Kauli hiyo siyo ngeni masikioni mwetu,tumekuwa tunaisikia mara kwa mara. Bila shaka wanaosema hivyo wamefanya utafiti na kugundua athari za vijana kutokuwa na ajira.

Haijalishi kama baadhi ya wanaosema hivyo kwa maslahi yao ya kisiasa kwa kutumia tatizo la ajira kwa vijana kama mtaji na daraja la kufikia malengo yao kisiasa badala ya uchungu unaotokana na kubaini madhara yanayoweza kutokea kwa kukosekana mipango na usimamizi kamambe wa kulijali kundi hilo kubwa la kijamii.

Lakini bado shaka waliyonayo ni yakweli na utabiri wao unaweza kutimia iwapo hazitachukuliwa hatua za haraka na madhubuti ya kuzuia hali hiyo ambayo binafsi siombei itokee. Niukweli usiopingika kwamba serikali imekuwa na mikakati na mipango kamambe ya kuwafanya vijana waweze kujiajiri.

Serikali kwa kutambua umuhimu na changa moto zinazozikabili kundi hili na wanawake imezitaka halmashauri kutenga asilimia kumi ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya mifuko ya vijana na wanawake.

Pamoja na sheria kuzitaka halmashauri kufanya hivyo lakini ni kama kuna mgomo baridi katika utekelezaji. Maana halmashauri nyingi hazitengi na kupeleka fedha kwenye mifuko hiyo kwa uwiano wa mapato yake ya ndani na kwa wakati.

Maana yake nikwamba mpango mkakati huo unabaki ni wakufikirika kama ilivyo kwa mipango mkakati na sera nyingine ambazo zinafanana na uzuri wa makaburi ambayo yamejengwa na kupambwa kwa marumaru lakini kilichomo ndani hakina uhai na kimeoza.

Kinachosababisha hali hiyo ni kukosekana kwa usimamizi madhubuti wa mipango na sera, ambazo zipo kwenye vitabu vilivyofungiwa makabatini na vishubaka. Hata hivyo wapo viongozi wachache miongoni mwa wengi ambao naamini wameliona tatizo lililopo na madhara yanayoweza kutokea iwapo uzembe katika kuzuia utaendelea.
mahiza Mkuu wa mkoa Lindi
Miongoni mwa hao wachache ambao wamebaini ukweli huo na kuanza kuchukua hatua kwa vitendo ni mkuu wa mkoa wa Lindi, Mwantumu Mahiza. Mkuu wa mkoa huyu miongoni mwa wakuu wa mikoa wachache wanawake, ambaye kama kumbukumbu zangu kama zipo sawa hajachukua hata miezi minne tangu ahamishiwe katika mkoa huu kutoka mkoa wa Pwani ameamua kufanya ambalo wengi walishindwa kufanya na bado wanashindwa kufanya iwe kwa uzembe, kutojua wajibu wao au kutojua madhara yanayoweza kutokea kutokana na kushindwa kuchukua hatua.'Eria kamishina (jina la kabla ya uhuru) huyu ambaye kwa sasa anaitwa rejino kamishina (mkuu wa mkoa) katika ziara zake za kujitambulisha, kutembelea na  kukagua shuguli mbalimbali za maendeleo katika wilaya za mkoa wa Lindi. Pamoja na mambo mengine alikuwa anasisitiza umuhimu wa halmashauri za manispaa, miji na wilaya zilizopo katika mkoa huu kutekeleza kwa vitendo agizo (sheria) ya kupeleka asilimia kumi ya mapato yake ya ndani kwenye mifuko ya vijana na wanawake na asilimia 60 zipelekwe kwenye miradi ya maendeleo.

Hiyo ilitokana na kutoridhishwa na utekelezaji wa sheria hiyo uliofanywa na halmashauri, ambazo ziliamua kutumia fedha hizo kwa shughuli nyingine au kukosekana kwa maelezo ikiwemo kuongezea katika Ujenzi wa Maabara kutekeleza Agizo Rais.

Katika kuonesha kuwa alikuwa hatanii (hakuwa na masihara) katika hilo alihaidi kuwaita vijana kutoka kila wilaya za mkoa huu ili wapewe mafunzo yatakayowazesha kuzitambua na namna ya kuzitumia fursa zilizo katika maeneo yao ili waweze kujiari na kujiletea maendeleo.

Huku akiwaagiza viongozi na watendaji kuwateua vijana bila ya upendeleo na itikadi za siasa, imani za kidini na ukabila wao. Binafsi niliamini  alikuwa anafanya siasa (porojo) kama ilivyozoeleka Kwa viongozi wetu walivyojaaliwa kuipepeta midomo yao na kuwapa wananchi matumaini yenye uzito mithili ya maputo.
mahiza Mkuu wa mkoa Lindi
Kumbe kama wenye busara zao wanavyotuasa kwamba mazoea siyo sheria na mtu haukumiwi kwa histora bali matendo ya wakati kwa makosa na mema ya wakati husika.

Mimi ni miongoni mwa wachache niliyekuwa naamini katika historia na mazoea katika kutoa hukumu. Nakiri kuwa nilifanya kosa kuamini hivyo Kwani Mkuu huyu wa mkoa alitimiza aliloliahidi kwa kufanikiwa kuwakusanya vijana 360 kutoka  katika halmashauri sita za mkoa huo. Ambapo walipata mafunzo kwa muda wa siku tano, kuanzia tarehe 23 hadi 27 Februari mwaka huu.

Vijana hao walipewa mafunzo ya ujasiriamali ikiwamo kutumia fursa zilipo katika maeneo yao, faida za kujiunga na mifuko ya kijamii, mifuko ya afya na namna ya kupambana na rushwa  Ambapo wataalam bobezi wa masuala hayo walitoa mada na hatimaye kufanya mijadala ya kina kuhusiana na mada husika zilizowasilishwa.

Kupitia semina hiyo baadhi ya Taasisi zimehaidi kusaidia mitaji na mikopo kwa vijana hao ambao ni mabalozi wazuri kwa wenzao ambao hawakushiriki semina hiyo.

Kwangu mimi kitendo hiki kilichofanywa na Mahiza ni cha kupongezwa na kupigiwa mfano Bila shaka kama viongozi na watendaji wetu watakuwa na mwenendo kama huu, tunaweza kufika pale ambapo wenzetu wamefika kimaendeleo na kuepuka tishio na kauli za kuwa ukosefu wa ajira kwa vijana ambao ni bomu linalosubiri kulipuka.

Nimalize makala yangu kwa kuomba vijana waliopata mafunzo hayo kuwa mabalozi wazuri watakao fikisha maarifa waliyopata kwa wenzao, wakati wakiyafanyia kazi kwa vitendo mafunzo hayo hasa baada ya kuwezeshwa mitaji na vifaa kama walivyohaidiwa.

Hakuna ubaya wakujifunza mambo mema, naamini viongozi wengine ambao hamjaanza kuchukua hatua mtakuwa mmejifunza kwa mkuu wa mkoa wa Lindi na muanze kuchukua hatua. Tatizo la ajira kwa vijana na wanawake linaweza kuepukika iwapo kutakuwa na utashi na dhamira ya kweli kwa viongozi wetu.

About Author

Advertisement

Post a Comment Blogger

Toa Maoni Yako Kuhusu habari Hii

Note: Only a member of this blog may post a comment.

 
Top