Man United yawekeza pauni 25 kujenga kituo tiba cha kisasa


132507_503269086351268_435842666_o LONDON, England
BAADA ya kumaliza msimu uliopita ikiwa na majeruhi wengi, Manchester United imeamua kuwekeza nguvu na akili zake katika kuondoa tatizo hilo.
Tayari, klabu hiyo imewekeza pauni 25milioni kujenga kituo cha kisasa cha tiba kwenye uwanja wake wa mazoezi Carrington.
Uamuzi huo unalenga kuipunguzia klabu hiyo gharama  ambazo inadai kuwa iliingia baada ya kumaliza msimu uliopita ikiwa na majeruhi wengi mno.
Kocha wao, Sir Alex Ferguson amekuwa akikabiliana na  tatizo la majeruhi wengi msimu huu ambao ni pamoja na Nemanja Vidic, Ashley Young na Phil Jones , wote hawajarudi uwanjani.


Kituo hicho kipya  na cha kisasa kinaifanya United kuwa ya kwanza duniani kuwa na kituo bora ambacho kitaweza kutambua majeraha kwa wanasoka pamoja na kufanya uchunguzi kama wa magonjwa ya moyo ambayo yanasumbua wanasoka kama Fabrice Muamba wa Bolton msimu uliopita.
Ukarabati wa kituo hicho ambao umegharimu karibu pauni  13m  umekamilika na  Man United imetangaza mpango wa miaka mitano wa kuingia mkataba  na  Kampuni ya Toshiba Medical Systems ya Japan  ambayo itatoa vifaa tiba ya pauni 12m.
"Nilidhani wanacheza, kumbe wanajenga kwa haraka," alitania Ferguson na kuongeza:"Lakini,Toshiba wameingia na wako tayari kuweka vifaa vya kisasa, hii ni hatua muhimu katika sayansi ya michezo na tiba kwa wachezaji wetu.
"Huu ni ushirikiano ambao utatuweka juu, mbali ya klabu nyinginezo duniani. Siamini kuwa Toshiba wanakuja hapa na vifaa vya kisasa vya tiba, bali kutusaidia. Tayari tunajivunia wataalam wazuri, ambao sina shaka watajifunia kufanya kazi kwa pamoja na Toshiba.
"Tatizo wakati mwingine ni kwa mashabiki ambao ni kama hawaoni uwekezaji huo. Lakini, tutaona faida yake, kila mmoja atafurahi. Haya ni maendeleo makubwa.
"Tumesajili wachezaji wengi mahiri msimu huu, lakini hawawezi kuwa wenye faida kama hawatakuwa fiti kucheza na kutoa matokeo mazuri."
Kituo hiki kitaiwezesha United kufanya uchunguzi wa afya ya wachezaji wake wapya na kutambua uwezo wao, aina za kudumu za majeruhi yao na hata mbinu za kuwatibu.
Previous Post Next Post