JAMII YAASWA KUENDELEA KUCHUKUA TAHADHARI KUJIKINGA NA MAGONJWA YA MLIPUKO

Jamii imeaswa kuendelea kuchukua tahadhari za kujikinga na Magonjwa ya mlipuko ikiwemo Marburg.

Hayo yamebainishwa na Afisa Lishe kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo Mkoani Kagera Bi.Domina Jeremiah wakati akitoa elimu ya Afya katika Kanisa la Waadventista Wasabato Ng'ambo.

Amesema miongoni mwa tahadhari muhimu za kuchukua katika kujikinga ni pamoja na kuwa na desturi ya kunawa mikono mara kwa mara kwa maji tiririka na kuepuka kusalimiana kwa kushikana mikono.


"Tunasema Kinga ni bora kuliko Tiba hivyo ni muhimu kuchukua tahadhari, tunawe mikono kwa maji tiririka na sabuni, tusisalimiane kwa kushikana mikono, pia toa taarifa kwa uongozi wa Kijiji, mtaa, Kituo cha Huduma za Afya kilichokaribu nawe au piga 199 bure" amesema.

Aidha, ametaja baadhi ya dalili za ugonjwa wa Marburg ni kutoka damu mwilini, Homa, kuhara au kuharisha damu na unaweza kuenezwa kwa kugusa majimaji ya mgonjwa ikiwemo jasho, damu, nguo, matandiko ya mtu mwenye maambukizi na kuchangia vitu vyenye ncha kali, maambukizi kutoka kwa wanyamapori ikiwemo sokwe, tumbili.

Mchungaji Samwel Mbilanga ni Mchungaji wa Kanisa la Waadventista Wasabato Ng'ambo Wilayani Biharamulo ameishukuru Serikali kwa kuweka jitihada kubwa za Utoaji wa Elimu ya Afya huku akisema Kanisa hilo limejizatiti katika masuala ya Afya.


"Tunashukuru Serikali kwa kuweka Kipaumbele cha elimu ya Afya ambapo na sisi kama Kanisa moja ya jambo kubwa tunalozingatia ni masomo ya Afya kanisani na tumehakikisha kuwa na ndoo za maji tiririka kila lango la Kanisa na chooni, na suala la ulaji huwa tunazingatia sana Afya" amesisitiza.

Aidha, Mchungaji Mbilanga amesema katika kipindi suala la maombi kwa kushikana wamesitisha ili kuzua maambukizi ya magonjwa ya mlipuko.

Katika utoaji wa elimu ya Afya kanisani hapo,baadhi ya wadau walioshiriki ni pamoja na Uwakilishi kutoka UNICEF, Africa CDC na TADIO.

Post a Comment

Hii ni Blog kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Nchi yetu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...

Previous Post Next Post