Waandamanaji nchini Misri wameshambulia makao makuu ya mgombea urais Ahmed Shafiq mjini Cairo.
Bwana Shafiq anashutumiwa kuunga mkono utawala wa zamani wa Bwana Mubarak, madai ambayo yeye na wafuasi wake wanakanusha vikali.
Uvamizi huo umetokea muda mfupi baada ya tume ya uchaguzi kuthibitisha kuwa uchaguzi wa marudio utafanyika mwezi ujao kati ya Bwana Shafiq, ambaye alikuwa waziri mkuu wa zamani katika utawala wa Rais Hosni Mubarak, na Mohamed Mursi wa chama cha Muslim Brotherhood.
Hakuna aliyedai kuhusika na mashambulio hayo.
Chanzo cha habari katika eneo la tukio kimesema jengo liliwaka moto kidogo, lakini halikupata uharibifu mkubwa.
Waandamanaji wapatao elfu moja wanaopinga matokeo ya uchaguzi huo pia walikusanyika katika medani ya Tahrir.