Unknown Unknown Author
Title: SIMULIZI:: SITALIA TENA SEHEMU YA 09
Author: Unknown
Rating 5 of 5 Des:
SIMULIZI:: SITALIA TENA SEHEMU YA 09 MTUNZI: NYEMO CHILONGANI ILIPOISHIA.....!!! “Mmh!” alijikuta akiguna, wakati huo, geti la kuingia k...
SIMULIZI:: SITALIA TENA
SEHEMU YA 09
MTUNZI: NYEMO CHILONGANI
SIMULIZI:: SITALIA TENA SEHEMU YA 09
ILIPOISHIA.....!!!
“Mmh!” alijikuta akiguna, wakati huo, geti la kuingia katika bandari hiyo likafunguliwa. Akahisi kuna tatizo, hakutaka kuondoka, alichokifanya ni kuligeuza gari lake na kuanza kurudi hukohuko. Alichohisi ni kwamba hata rafiki yake, Yusuf Al Sadiq alikuwa amemsaliti kama alivyomsaliti Al Khalid.

ENDELEA NAYO SASA....
Haikuwa kawaida kwa polisi kufika bandarini, kila mmoja alishangaa kwani polisi hao hawakuruhusiwa kuingia humo mpaka pale watakapokuwa na kazi maalumu, hasa kama kulikuwa na meli iliyoingia ambayo walihisi kwamba ilikuwa na madawa ya kulevya.

Siku hiyo, hakukuwa na meli yoyote iliyoingia kitu kilichowafanya watu wote kushangaa sababu ya polisi hao kufika humo. Mara baada ya kuyapaki magari yao wakateremka na kisha kuanza kuelekea katika ofisi ya mkuu wa bandari hiyo, walitaka kuzungumza naye kwani walihisi kulikuwa na kitu hakipo sawa.

Kareem hakutaka kuondoka, alijua kabisa kwamba sehemu hiyo haikuwa na usalama wa maisha ya mpenzi wake, alichokifanya ni kuteremka na kisha kuanza kurandaranda ndani ya bandari hiyo.

“Ulilisikia tangazo?” aliuliza mkuu wa polisi.
“Tangazo lipi?” aliuliza mkuu wa bandari.
“Kwamba hakutakiwi meli yoyote kuondoka mpaka ifanyiwe upekuzi!”
“Hapana, sikusikia. Kuna nini kwani?”
“Hujui kama kuna msichana ametoroshwa?”
“Msichana kutoroshwa! Wapi?”

Wakaanza kumwambia, alionekana kutokufahamu kitu chochote kile kilichokuwa kikiendelea. Alimwangalia polisi huyo, alimshangaa kwani aliamini kwamba kwa kipindi chote ambacho magaidi na watu wengine walipokuwa wakitoroka, hawakupitia katika bandari hiyo, wengi wao walipita jangwa kwa jangwa mpaka kuingia nchi nyingine.

Hakuwakatalia, akakubaliana nao kwamba ilikuwa ni lazima kila meli ichunguzwe kwani walihisi kwamba inawezekana msichana Saida alikuwa akitoroshwa kupitia bandarini hapo.

“Haiwezekani kuwa hivyo!” alisema mkuu wa bandari.
Polisi wale hawakutaka kuchelewa, walichokifanya ni kuanza upekuzi kama ilivyokuwa. Kulikuwa na meli nne ambazo zilitakiwa kuondoka siku hiyo, wakaanza na meli ya kwanza, walipekua kila sehemu, tena kwa uangalifu mkubwa, kwa kule walipoambiwa kwamba kulikuwa na mizgo tu, hawakukubali, napo wakaelekea huko na kuanza kupekua.

Walipomaliza meli tatu ndipo wakaamua meli ya nne ambapo ndipo alipohifadhiwa Saida, hakukuwa na mfanyakazi yeyote aliyekuwa akifahamu uwepo wa mtu huyo ndani ya meli hiyo zaidi ya Yusuf Al Sadiq ambaye alijitahidi kumuingiza msichana huyo katika sehemu ya mizigo ambayo ilikuwa na mapipa mengi ya chokaa.

Wakati upekuzi katika meli yake ukiendelea, Yusuf Al Sadiq alionekana kuwa na hofu, alijua kwamba msichana aliyekuwa akitafutwa alikuwa ndani ya meli yake. Hakutulia, kila wakati alionekana kuwa na hofu, hakutaka kabisa msichana huyo aonekane kwani alijua kwamba kama angeonekana basi hata yeye angeshitakiwa kwa kutaka kumtorosha mtu aliyekuwa akitafutwa na serikali.

“Yusuf Al Sadiq, nini kinaendelea?” aliuliza Kareem huku akimwangalia Yusuf Al Sadiq.
“Polisi wamekuja kupekua.”
“Kupekua nini?”
“Wanataka kuona kama kuna msichana wako!”
“Ila si yupo ndani?”
“Ndiyo! Yaani hapa sijui nifanye nini!” alisema Yusuf Al Sadiq huku akitetemeka, kwa jinsi alivyoonekana tu, alionekana kuwa na hofu kubwa.

Polisi hawakujali, bado waliendelea kumtafuta Saida ndani ya meli hiyo. Hawakutaka kusikia lolote lile kutoka kwa mtu yeyote, walikuwa mahali hapo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba meli zilizokuwa zikiondoka hazikuwa na mtuhumiwa ambaye kipindi hicho alionekana kuwa dili.

Wakati hayo yote yakiendelea, Saida alikuwa ndani ya chumba kilichokuwa na mapipa yaliyojazwa chokaa iliyochangwa na maji tayari kwa mtumizi na ilikuwa ikisafirishwa kuelekea Dubai kwa ajili ya kupaka katika jengo refu la Al Sultan lililokuwa mjini humo.

Wakati akiwa humo, akasikia watu wakija kule alipokuwa, moyo wake ukamripuka, hakuona kama kweli angeweza kusalimika. Alitamani kujificha lakini hakukuwa na sehemu ya kujificha, aliyaangalia mapipa yale, yote yalikuwa na chokaa iliyokuwa imewekwa katika maji na kuyafanya mapipa hayo yote kujaa.

“Nitajifichia wapi?” alijiuliza, ndani ya chumba hicho hakukuwa na kitu kingine zaidi ya mapipa hayo tu.

Wakati akijifikiria nini cha kufanya ili kujiokoa, vishindo vya watu hao vikaja mpaka nje ya mlango ule, akabaki akitetemeka, alisimama huku kijasho chembamba kikianza kumtoka.
“Kuna nini humu?” aliisikia sauti ya mwanaume mmoja, alihisi kwamba alikuwa polisi.
“Mizigo kwenda Dubai!”
“Mizigo gani?”
“Mapipa ya chokaa!”
“Nataka niyaone..” alisikika mwanaume huyo.
“Sawa!”
“Fungua mlango!”

Saida aliyasikia vilivyo mazungumzo hayo, alibaki akitetemeka tu. Vijana hao ambao walitangulizana na polisi mpaka katika mlango wa chumba hicho hawakujua kitu chochote kile, bosi wao hakuwaambia kama humo ndani kulikuwa na mtu aliyekuwa akimsafirisha.

Muda wote huo Saida alikuwa chumbani kwake, alikuwa akilia kwani hakuamini kama kweli huo ndiyo ulikuwa mwisho wake. Alimuomba Mungu aweze kumtoa ndani ya nchi hiyo salama, hakuwa na tumaini lolote zaidi ya Mungu tu.

Wakati akihuzunika ndani ya chumba hicho, mara akasikia mlango wa chumba hicho ukifunguliwa. Ulikuwa mlango mkubwa ambapo kuufungua ilitakiwa uchukue dakika moja kuufungua wote.

“Nimekwisha...” alisema Saida, baada ya dakika moja, mlango ukafunguliwa na polisi wote kuingia ndani ya chumba hicho.

***********************
Wote walibaki kuwa na wasiwasi, walijua tu kwamba ilikuwa ni lazima Saida akamatwe kwani tayari polisi wale waliingia ndani ya chumba hicho. Kareem ndiye aliyekuwa na hofu zaidi, kwa Saida, kwake alikuwa kila kitu, alimpenda na alimthamani kuliko mtu yeyote na zaidi ya hilo ni kwamba alikuwa na mtoto wake tumboni.

Hakutaka kuona hilo likitokea, hakutaka kuona mpenzi wake akikamatwa na kwenda kunyongwa au kupigwa mawe, kwake, ilikuwa ni lazima kupambana ili kuiokoa familia yake, kama kuweka uadui na nchi yake, alikuwa tayari kwani hata Mrusi Victor Belenko aliisaliti nchi yake mwaka 1976 kwa kuipeleka Japan na watu hao kuchukua njia zilizotumika kutengeneza ndege hiyo ya kijeshi.

“Kama Belenko aliisaliti nchi yake, kwa nini nishindwe?’ alijiuliza Kareem.
“Unamaanisha nini?”
“Naweza kupata bunduki?” aliuliza Kareem huku akimwangalia Yusuf Al Sadiq.
“Bunduki?” aliuliza Yusuf Al Sadiq huku akishtuka.
“Ndiyo!”
“Hapana! Hapa nina bastola tu! Unataka ya nini?”
“Maswali ya kijinga Yusuf Al Sadiq. Kwani kazi yake nini? Nipe hiyohiyo bastola,” alisema Kareem, kwa siri kubwa Yusuf Al Sadiq akampa bastola Kareem.

Akasimama huku akitetemeka kwa hasira, alikuwa akiwasubiria polisi wale waliokwenda ndani ya meli ile na kuingia ndani ya chumba kile. Kwa kipindi hicho, alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile lakini si kumuona mpenzi wake, Saida akichukuliwa na polisi hao.

Wala hazikupita dakika nyingi, polisi hao wakatoka ndani ya meli ile, mkuu wa polisi wale walioingia ndani ya chumba kile wakawa na tabasamu pana kwa kuonyesha kwamba kila kitu kilikuwa kimekamilika, walifanya kile kilichotakiwa kufanywa.

“Let me go...” (niache niondoke) ilisikika sauti ya msichana mmoja aliyekuwa ameshikwa na polisi hao. Kareem alipomwangalia msichana huyo, hakuamini macho yake.

Akajiweka vizuri na kuuficha mkono uliokuwa na bastola ile.

Je, nini kitaendelea?
Je, nini kitatokea baada ya Saida kukamatwa?
Tukutane Saa moja Jioni.

About Author

Advertisement

Post a Comment Blogger

Toa Maoni Yako Kuhusu habari Hii

Note: Only a member of this blog may post a comment.

 
Top