TANZIA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA BUNGE LA TANZANIA

Spika wa Bunge, Mhe. Anne Makinda, (Mb) anasikitika kutangaza kifo cha Mbunge wa Chambani, Pemba, Mhe. Salim Hemed Khamis (CUF) kilichotokea leo mchana katika Hospitali ya Taifa Muhimbili. Marehemu Khamis, alilazwa jana katika Hospitali hiyo baada ya kuanguka ghafla akishiriki vikao vya kamati za Bunge vinavyoendelea katika Ofisi Ndogo ya Bunge, Dar es Salaam.

Marehemu ambaye alikuwa mjumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, alikimbizwa Hospitalini na kulazwa katika chumba cha wagonjwa Mahututi Muhimbili baada ya kubainika kuwa alikuwa amepata kiharusi kufutia shinikizo la damu lililopelekea kuanguka kwake ghafla akiwa katika majukumu yake katika Kamati za Bunge. Kutokana na Msiba huu, Shughuli zote za Kamati za Bunge zimearishwa hadi jumanne tarehe 2 Aprili, 2013.

Marehemu ataangwa kesho tarehe 29 Machi, 2013 saa mbili na Nusu Asubuhi katika Ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam na kusafirishwa kwa ndege kwenda Pemba Saa Nne Asubuhi ambapo Mazishi yatafanyika nyumbani kwake Chambani, Pemba Mchana. Mhe. Spika anatoa Pole kwa Familia ya Marehemu, wananchi wa Chambani, Wajumbe wa Kamati ya Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, Wabunge wote na Watanzania wote kwa ujumla.

Mungu alilaze Roho ya Marehemu, Mahali Pema Peponi, Amina!

 

Imetolewa na

Idara ya Habari, Elimu Kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa

Ofisi ya Bunge

DAR ES SALAAM

28 Machi, 2013

Post a Comment

Hii ni Blog kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Nchi yetu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...

Previous Post Next Post