Unknown Unknown Author
Title: RIWAYA: SITASAHAU FACEBOOK SEHEMU YA ISHIRINI
Author: Unknown
Rating 5 of 5 Des:
RIWAYA: SITASAHAU facebook MTUNZI: Emmy John P. SEHEMU YA ISHIRINI Nikatazama juu nikakutana na mawingu yenye rangi inayoshabihiana na buluu...

FACERIWAYA: SITASAHAU facebook
MTUNZI: Emmy John P.
SEHEMU YA ISHIRINI
Nikatazama juu nikakutana na mawingu yenye rangi inayoshabihiana na buluu, nikaikumbuka rangi ya mtandao wa kijamii. Ni huku nilikutana na Dokta Davis. Akanipa zawadi ya utajiri, akanipatia kazi nyepesi inayonipatia kipato kikubwa. Nikamuamini sana. Sasa alikuwa amegeuka joka kubwa na lilikuwa linaniua.
Hakika lazima nife!! Jitihada zangu zote hazikuwa na maana tena.
John hakuwa msaada wowote kwangu. Na hakuwepo mwingine wa kunipa msaada.
Nilipofikiria ni nani mwingine wa kunisaidia akili yangu ikarejea kwa mwalimu Nchimbi. Mama yangu mzazi. Nikajaribu kuita sauti haikutoka. Mama naye hakuwa na msaada katika hali hii.
Nikayakumbuka maneno ya mama. Miaka mingi sana nikiwa mdogo aliwahi kunikambia maneno.
“Yupo mtu anakusikia hata usipotoa sauti.” Hili lilikuwa jibu alilonipa baada ya kumuuliza iwapo mabubu na viziwi wanaweza kuzungumza na Mungu. Jibu lake hadi ukubwani halikunitoka.
Nami sasa nilikuwa bubu. Jaribio la mwisho kabisa ni kuzungumza na yule anayesikia wakati wote. Ajuaye unachokiwaza. Kila wakati, mahali popote.
Mungu!
“Eeh! Baba sijui kama nilistahili adhabu hii. Na kama ilikuwa stahili yangu baba. Nichukue kwako sasa. Nimeumia na IMETOSHA.” Nilizungumza katika nafsi yangu. Kisha nikasubiri kuiaga dunia hii chungu.
Nilitua chini kama mzigo mzito, bahati nzuri nilitua katika majani. Sikuumia. Nilipumua kwa fujo sana, nilikuwa nimerejewa na uhai tena.
Nikalishuhudia lile joka likihangaika huku na huko, hatimaye likatoweka.
Maajabu makubwa ambayo sijapata kuyaona na yalikuwa yanastahili kutolea ushuhuda.
Sikuwahi kuwa na imani katika miujiza lakini sasa ilinitokea ili niiamini. John naye alikuwa anashangaa kama awali. Na bado hakuweza kuniona. Sikupoteza muda nikamshika mkono. Tukaanza kuondoka. Sikukiacha kisu changu.
(HARAKATI NDOLLA ZAMBIA)
Nilijikuta naifuatilie ile njia tuliyopita awali hadi nikaufikia ule mlango. Nikamtanguliza John nami nikatoka.
Maajabu mengine. Niliwakuta wale waliotangulia wakiwa katika sintofahamu wasijue nini cha kufanya.
Kwa kukadiria muda ilikuwa saa sita mchana. Na tulikuwa katika ulimwengu halisi lakini hatukutambua ni wapi hapo tulipo.
Magu, Bariadi, Sumbawanga, Songea!! Kila mtu alifanya utabiri wake.
Hatukuendelea kukaa pale. Tukaanza safari kuelekea tunapoelekea bila kutambua ni wapi.
Baada ya kilometa takribani sita tukaingia kijijini.
Mimi nikiwa na upande wa kanga pekee. Wenzangu wakiwa na nguo zilizochakaa sana. Tukakiona kijiji. Baadaye tukaanza kukutana na watu.
Kila mtu akiwa na lake la kufanya. Hakuna aliyetuuliza swali. Walikuwa weusi sana, wengine walifanana na nyani huku wanawake wengi wakiwa na maziwa makubwa.
Ni wapi sasa hapa? Nilijiuliza.
Tulitamani sana kuzungumza na watu hawa lakini hawakuwa wakarimu.
Njaa iliuvunja uamuzi wetu wa kusubiri watuanze. Njaa ilituuma na hatukuwa na chochote cha kuweka tumboni.
“Ha…habari..”
“Nkesuu…” sijui kama aliniuliza ama alinijibu salamu.
Lugha ya wapi hii!! Niliwahi kusikia mahali, ni wapi vile. Niliumiza kichwa. Kila mmoja alikuwa ananitazama mimi kama mwokozi katika mapambano haya.
“Me come great…” nilizungumza kiingereza kibovu ili nipate kujua wanazungumza lugha gani na ni watu wa wapi. Hakunijibu akanikazia jicho kwa shari. Ni hapo nikapata jawabu sura hizi nimewahi kuziona wapi. Ni kwenye basi. Siku ya safari yangu kuelekea Ndolla Zambia kwa Dokta Davis kusaini mkataba ule ulionifikisha hapa nilipo.
“Sam…it’s either Congo or Ndolla….(Sam ni aidha Kongo ama Ndolla)” nilimnong’oneza yule msukuma.
“Ndolla??”
“Yes! Ndolla Zambia..” nikamjibu. Akashangaa. Yule bwana tuliyemuuliza akawa amesonya na kutoweka.
Watu hawa sio wazuri hata kidogo. Wameathiriwa na vita za wao kwa wao. Wakitugundua ni hatari. Naamuru!! Hakuna mtu kuzungumza na mgeni yeyote, I WILL!!! Nilitoa tamko kama amiri jeshi mkuu wa mapambano hayo.
Kila mmoja akanielewa.
Safari ikaendelea, tulikuwa tumechoka lakini tuliuhitaji sana ukombozi, tulihitaji uhuru wetu.
NDOLLA TOWN 40 KM AHEAD. Kilisoma hivyo kibao kigumu cha chuma. Nikajipongeza katika nafsi yangu kwa kuwa na kumbukumbu nzuri.
Jesca alikuwa mtu wa mawazo mazito. Hakuwa akiongea na ule urembo wake wa enzi zile haukuwa na nafasi hapa. Pia ugomvi wetu wa kumuwania John kimapenzi haukupewa nafasi pia. Kila mmoja alitazama anajikomboa vipi.
Tulitembea kimafungu mafungu. Jumla tulikuwa watu ishirini na moja lakini, tulikuwa kama hatufahamiani. Kila mmoja na lake. Likitokea la kuzungumza nilikuwa nachukua nafasi hiyo.
Tulipoufikia mto, kila mmoja aliyatumia maji anavyoweza, wengi walikunywa na wachache walioga. Pumziko la dakika ishirini kisha tukaendelea mbele. Tukaufikia mti wa maembe. Hapa sasa kila mtu alikula kulingana na ukubwa wa tumbo lake. Angekuwa mjinga ambaye angeacha kubeba akiba ya maembe matamu ya Zambia.
Sasa kasi ikaongezeka na mazungumzo yakaibuka. Njaa kitu kibaya sana.
Mimi na John tulikuwa tumeambatana. Ile hali ya yeye kutoniona iliniumiza sana lakini sikuwa na namna.
Kilometa zikazidi kukatika, tulitembea hadi usiku, kwa kukadiria tulitumia masaa yanayozidi kumi. Kuzikamilisha zile kilometa.
Mji wa Ndolla ukatukaribisha. Ulikuwa mara yangu ya pili kuja katika mji huu na mara ya kwanza kufika nikiwa katika matatizo.
Nilijipongeza tena kwa tabia yangu niliyoionyesha siku ya kwanza. Tabia ya kushangaa shangaa. Hivyo kuna baadhi ya vitu nilivikumbuka. Hadi tukaipata stendi.
Kama nilivyoamuru kila mmoja alijitenga kama hatujuani. Kanga yangu ikiwa imefungwa vyema. Ni hiyo pekee ilikuwa ngao yangu. Nikaingia katika stendi ile ambayo ilikuwa inazidiwa hadhi na stendi ya Ubungo jijini Dar es salaam katika nchi yangu ya Tanzania.
Nilizunguka hapa na pale. Nikaiona ofisi ya magari ambayo nilikuwa naitaka.
“Mambo vi wewe…inakuwaje…mishemishe vipi…oya acha kuzingua…” maneno haya yalikuwa yanazungumzwa katika ofisi hizi.
Nikainama chini jicho langu la kulia likatangulia kumwaga chozi la kushoto nalo kwa uchungu likamwaga chozi. Nikajiinamia chini nikalia kwa uchungu mkubwa. Uchungu wa kuikumbuka nchi yangu Tanzania. Kilio hichohichoi kwa namna ya kipekee kilikuwa kilio cha furaha. Ndio lazima nifurahi. Sasa ningeweza kumvuta mtu na kuzungumza naye Kiswahili.
Ni hivyo nilifanya. Mwanaume kipande cha mtu akavutika kunisikiliza. Kwanza sikutaka kumuelezea kuwa tupo wengi. Niliitetea nafsi yangu. Nilikuwa natetemeka kwa baridi. Akanipatia sweta zito nikajistiri. Nikajielezea kuwa nimepotezana na bwana aliyenileta Zambia.
“Umesema wewe mwenyeji wa Makambako.”
“Ndio kaka.”
“Makambako sehemu gani hiyo?”
“Ni karibia na stendi kuu. Hapa Magegele …..”
Alaa Magegele napafahamu sana huko…kabla ya kuhamia huku nilikuwa naenda na mabasi ya Dodoma Mbeya…sasa hapo Magegele kuna mgahawa tulikuwa tunakula tulimzoea sana yule mama kiukweli..hata wewe nikutajia lazima utakuwa unamjua..”
“Mama Kesho.” Niliwahi kumjibu. Akacheka sana, hakuna mtu wa Makambako ambaye hakumjua mama huyu. Alikuwa mkarimu sana.
Tulizungumza mambo mengi usiku ule. Alizungumza nami kwa ukarimu. Ni nani alikwambia kuwa watanzania sio wakarimu.
Kuna tofauti kubwa kati ya mtanzania na mbongo!! Mtanzania ana utu lakini mbongo anajifanya mjanja mjanja. Huyu bwana alikuwa mtanzania haswaa.
Upesi nikapata chakula. Kisha akaingia ndani akatoka na nguo. Zilikuwa za kike.
Akanieleza abiria huwa wanasahau nguo zao na kamwe hawarudi tena kuzichukua. Nikamshukuru. Akanipatia na kiasi cha pesa. Akaniomba nirejee majira ya saa tano asubuhi aweze kunifanyia utaratibu wa kunisafirisha kurejea Mbeya kisha Makambako Iringa.
Ilikuwa bahati ya kipekee sana kupata msaada huu. Lakini hapo hapo ilikuwa bahati mbaya sana maana nisingeweza kusafiri peke yangu. Na yule bwana sikumueleza tupo wengi zaidi ya kikosi cha timu ya mpira wa miguu.
Ubarikiwe sana!! Nilimpa Baraka hizo.
Kisha nikiwa na mavazi kamili sasa. Nikapiga hatua kwa hatua. Kigiza giza kikanifanya nionekane kama kivuli. Mkono mmoja mfukoni kuzilinda Kwacha (Pesa halali kwa matumizi ya Zambia) nilizopewa, mkono mwingine ukiwa umeshika kiroba cha nguo nilizopewa na yule bwana. Isabela nikiwa na raba nyepesi miguuni. Nikatoweka huku nikiamini nina mzigo mkubwa wa kuwaokoa rafiki zangu ambao walinitazama kwa jicho la huruma.
Nilijihesabu kama mshindi wa vita ya 666. Lakini bado nilikuwa na vita nyingine ya kurejea nyumbani.
Mshindi akifia ugenini huyo ni mshindwa lakini akirejea nyumbani hata kama amejeruhiwa vipi bado ataitwa mshindi.
Mapambano yameanza rasmi!!! Nilikiri huku nikiwa nayatamani hayo mapambano ambayo yatakuwa magumu kushinda vita ya joka kuu la msituni.
Nilimchukua Jenipher, Jesca na Samson. Kikawekwa kikao cha dharula. Mada kuu ikiwa tunatoka vipi.
Nilimpatia Jenipher na Jesca baadhi ya nguo. Wakajihifadhi.
Mazungumzo yalikuwa marefu sana na pambazuko lilikuwa linakaribia. Mengi yalizungumzwa na sasa tukawa tumefikia katika maamuzi mawili. Kubwa kabisa likawa kukimbilia ubalozini kupata msaada.
Wazo la kupata simu tuweze kufanya mawasiliano nyumbani pia lilitujia vichwani!! Lakini hatukulitilia sana maanani katika nchi za kigeni. Tulitaka tufike kwanza Tanzania ndipo tufanye mawasiliano.
Ubalozini!! Hiyo ndio ikawa mada.
Lakini swali likaja kwa John ambaye bado alikuwa na alama 666 na hakuwa akionekana. Lakini kama hiyo haitoshi, tukapata hofu ya usumbufu wa maswali mengi kutoka kwa chombo husika kitakachokuwa kinahusika na mambo ya uhamiaji.
Kwa jinsi tulivyokuwa wengi tuliamini kuwa itatuwia ngumu sana kupata msaada upesi. Pia ubalozi wa Tanzania katika nchi ya Zambia ulikuwa una makao yake Lusaka. Mji mkuu wa Zambia.
Hilo lilikuwa gumu sana. Tulikuwa tunahitaji pesa. Pesa!!
Kama tukipata pesa tunaweza kupanda mabasi yatakayotufikisha Mbeya. Hapo sasa tutakuwa katika ardhi salama ambayo tunaweza kupata msaada.
Pesa tutaitoa wapi? Hilo likawa swali.
Tukakubaliana kuingia katika mapambano ugenini. Mimi, Jesca, Jenipher na Samson. Tukafunga mjadala.
Asubuhi ikazidi kujongea. Hapa sasa nikachukua maamuzi. Nikatembelea kundi moja baada ya jingine. Nikawapatia chakula kidogo kidogo nilichonunua kwa kutumia pesa niliyopewa na kaka yule wa kitanzania. Huku katika kila kundi nikiwapa moyo kuwa tumekaribia kuondoka kurejea nyumbani.
Siku iliyofuata kila mtu alikaa kwa tahadhari bila kuzungumza na raia wa Zambia.
*****
Majira ya saa nne asubuhi nilikuwa katika ofisi ya yule mwanaume wa kitanzania aliyeahidi kunisaidia niweze kufia Mbeya. Nilimkuta akiwa amebanana kulingana na majukumu. Nikatulia mpaka alipomaliza. Nikaingia.
Alinichangamkia sana. Akamkabidhi mwenzake ofisi akanipeleka mgahawani. Chai ya maziwa na chapatti nzito kabisa.
Mazungumzo yakiendelea!!!
Akanielezea mpango wake huku akinisihi niwe mvumilivu katika safari maana patakuwa na tatizo la kuhamishwa siti na wakati mwingine kukosa kabisa pa kukaa maa nitasafiri kama ‘staff’. Hilo halikuniumiza kichwa sana, maana niliamini naweza kusimama cha msingi nia yangu kutimia. Kilichoniumiza kichwa ni hawa wenzangu. Itakuwaje!!
Nilimshukuru yule bwana. Akanipatia namba yake ya simu. Ni hapo nilimtambusa jina lake aliitwa Saidi.
“Ukinipigia simu we niite Side boy.” Aliniambia wakati ananiaga.
Alinipatia kiasi kingine cha pesa.
Nilishukuru kwa kuzaliwa mwanamke maana bila hivyo sidhani kama ningepata msaada.
Jioni ilipofika. Jesca hakuwa ameambulia lolote. Na Sam hadi wakati huo hakuwa amerejea. Tukajipa moyo kuwa huenda amefanikiwa kupata kibarua chochote huko alipo. Ikafika giza nab ado Sam hakuwa amerejea. Hofu ikaanza kutuingia na kuamini kuwa Sam anaweza kuwa aliongea Kiswahili na kugundulika kuwa ni mtanzania asiyekuwa na uhalali wa kuishi Zambia.
Hatukujua kuwa ni wapi tuanzie kumtafuta. Kama tukisema twende polisi na sisi tutakuwa matatani. Tatizo jipya!!
Jesca na Jenipher wakawa wananisikiliza mimi.
Kimya kikatanda!! Makundi mengine hayakujua nini kinaendelea.
Nilijiuliza maswali mengi sana bila kupata majibu. Samson amefanya jambo gani la kitofauti hadi wakati huu hajarejea.
Au amerejea tena katika kijiji cha Dokta Davis. Niliwaza peke yangu bila kumshirikisha mtu yeyote hisia zangu.
Saa nne usiku nilikuwa nimepitiwa usingizi.
Nilisikia kama natikiswa nikadhani ni Jesca amejigeza lakini nilikuwa naendelea kubughuziwa. Japokwa nilikuwa nimelala chini niliutamani usingizi.
Nilijikaza nikafumbua macho.
Usingizi ukakatika palepale. Alikuwa ni Sam!!
“Bella!! Bella!!” alinong’oneza. Nikamtazama usoni nikahisi kuna nhali ya tahadhari. Nikajipa utulivu wa lazima.
Akanishika mkono akaninyanyua. Akanivuta pembeni kidogo.
“Ulikuwa wapi Sam.”
“Bwana Mkubwa!!.”
“Kafanyaje…ndio nani?” nilitaharuki.
“Sio mtu ni sehemu inaitwa hivyo.”
“Pamekuwaje…”
“Nimekutana na mtu!! Aah!! Nimemuona mtu….amepata madini.”
Bado sikuweza kumuelewa Sam anamaana gani. Nikamuomba anielezee kwa kirefu.
Akanieleza juu ya mgodi wa Bwana Mkubwa ambao upon je kidogo ya mji wa Ndolla. Mgodi huu alipoutaja tu! Sikuwa na swali lolote. Nilikumbuka somo la Historia kidato cha pili hadi cha tatu. Mgodi huo ukanikumbusha madini hadimu ya Risasi (Copper) ambayo hupatikana kwa wingi katika nchi ya Zambia. Hasahasa Ndolla.
Sam akaendelea kunielewesha. Na sasa akanigusia juu ya bwana ambaye amepata madini hayo siku hiyo.
“Kwa hiyo ulikuwa huko.”
Akanijibu kwa kutikisa kichwa juu na chini akimaanisha kuwa ni kweli alienda ‘Bwana Mkubwa’.
Samson alikuwa amekuja na habari ambayo mwanzoni nilikuwa ninapingana nayo lakini hatimaye kulingana na shida tuliyokuwanayo nikaamua kukubaliana naye. Wizi!
Samson alinihakikishia huyo bwana ana pesa nyingi sana. Amefuatilia nyendo zake hadi alipofanikisha kuyauza yale madini.
“Alinipa lifti kwenye gari yake. Nilijifanya sijui lolote lile. Aliponishusha mjini nikamfatilia na kumuona aliyauza.”
“Sasa tunampata wapi?”
“Yupo anakunywa pombe sasa hivi. Ni hapo pekee pa kumkamatia.” Alinisisitiza.
“Nzuri zaidi ni mtanzania…” alinisisimua kwa kauli hiyo. Nikamwomba Mungu huyo bwana asiwe na tabia za kitanzania bali awe mbongo.
Nilitulia kwa dakika chache kisha nikamuamsha Jesca. Hakunisikia. Nikapekua huku na huko. Nikachukua mafuta. Nikaenda bafu za kulipia nikaoga. Nikajipaka mafuta. Nikavaa kanga moja.
Samson akawa kioo changu akakiri kuwa kwa namna ile lazima anitamani.
Samson akaniongoza hadi nikafika eneo la tukio.
Jirani na bwana huyu palikuwa na kiti kipweke ambacho hakikuwa na mlevi aliyekikalia. Nilikitoa upweke nikajiweka juu yake.
Haraka akafika muhudumu wa kizambia, mweusi na mbaya kumtazama. Nikaagiza soda.
Meza yangu haikuwa mbali sana na yule bwana ambaye Samson alinielekezea. Nilikunywa soda taratibu huku nikiisoma akili ya yule bwana aliyepata bahati ya kupata madini Bwana mkubwa.
“Yaani wahudumu wengine nao….ona sasa.” Nilizungumza kwa hasira. Kama najiongelesha. Sauti ikamfikia mlengwa ambaye ni yule bwana anayekunywa pombe.
Akajileta mtegoni.
Akasogeza kiti karibu nami.
“Wewe ni mtanzania kumbe..ama unaibiaibia Kiswahili. Nimefurahi kukusikia ukisema Kiswahili.”
Nikatabasamu, nikalegeza jicho kimaksudi.
“Yeah! Mtanzania halisi…..na wewe je?”
“Mimi ndio orijino kabisa.” Alijibu. Nikacheka tena.
“Dah!! Miezi miwili sijarudi nyumbani aisee. Maisha haya.” Nililalamika.
“Aaah! Mimi kila wiki huwa naenda aisee.”
Maongezi yakawa maongezi. Kama bahati alinipendelea vile. Yule bwana alikuwa na tabia za kibongo. Akaniingizia mada za mapenzi.
Sasa nane usiku tukawa tunatafuta chumba kwa ajili ya kutimiziana haja. Yeye akinitaka kimwili na mimi nikimtaka kipesa.
Alilipia chumba cha bei ghali sana. Nilimshuhudia wakati anauacha mkoba wake mapokezi. Nikagundua mchezo unataka kuharibika.
Nikajipa moyo. Nikaenda hadi chumbani!!
Hapakuwa na jipya huko. Mzee huyu mwenye matamanio. Alinivagaa na kuanza kunisumbua huku na huko. Sikuwa na hisia hata kidogo. Niliwaza pesa tu.
Nilipomtazama umri wake nikagundua huyu hana lolote la kuweza kunishinda. Akili ya maajabu ikanivaa, nikajikuta nimevamiwa na wazo kuwa kama nisipokuwa makini naweza kutumika kimwili na nisipate chochote kile.
Nikaamua kutumia nafasi moja tu kusawazisha mambo haya!!!
Pata potea!!
“Mh!! Hauna kinga?” nilimuuliza baada ya kuwa nimempelekesha akalegea kabisa macho yake na nikajua kuwa alikuwa anahitaji mwili wangu.
Ni hapa nilikuwa napahitaji.
“Sina mpenzi wangu…njooo tu hivyo hivyo” akajibu. Nikamtukania mama yake kimoyomoyo kwa ujinga aliozaa.
Nikasimama. Nikamtazama kwa jicho la kimapenzi huku moyo wa chuki ukimtusi. Ubongo unaohitaji pesa nao ukifanya kazi kwa bidii kubwa.
“Ngoja niende kuchukua mpenzi wangu, naogopa mimba mwenzako, ujue nimeolewa eeh!!” nilimlaghai. Akaingia mkenge. Nikachukua upande wangu wa kanga, nikashusha ngazi mpaka mapokezi.
Nikamkuta mwanadada mweupe akiwa ameuchapa usingizi.
“Nipatie mkoba wa mzee!!” nilimwambia huku nikiwa nimetega mkono!! Moyo ukiwa hauamini kama nitafanikiwa.
“Mmm. Hapana mwambie aje mwenyewe dada, hajaturuhusu kumkabidhi yeyote zaidi yake.” Alinipinga yule dada kwa kingereza chake kibovu kisha akaendelea kuuchapa usingizi. Nilitamani sana kumrukia nimkabe. Lakini alikuwa ametenganishwa na nondo. Nisingeweza hata kumgusa.
Niliondoka pale nikiwa nimetaharuki sana, mpango ulikuwa unakaribia kushindikana sasa, na asubuhi inayofuata nilitakiwa kusafiri kuelekea Mbeya.
Nikapanda hadi juu kule chumbani nikaufungua mlango kwa ghadhabu kubwa.
Yule bwana akashtuka.
“Ndio ujinga gani huu huku Zambia I hate such embarrassment!!” nililalamika.
“Nini tena mamito.” Aliniita kimapenzi akiwa amelegea.
“Yaani hadi kuchukua kinga I need to go with you!!”
“He!! Wamekunyima?” aliponiuliza swali hilo, nikajikuta Napata nafasi ya mwisho.
“Fanya hivi naomba umpigie umwambie anipe!! No discussion!!” niliwaka, zile hasira za kutaka kuikosa pesa ile zilikuwa zimenipanda.
Mbongo akachukua simu akainyanyua. Nikaomba mizimu yote asije akasemam maneno mengi kwenye simu.
“Halo!! Chumba namba 12….mpe huyo dada nilichomuagiza…na muache mambo ya kipumbavu” akakoroma kwa kiingereza kilichonyooka. Kisha akakata simu kwa hasira.
Sikusema neno!! Nikafungua mlango, nikatoka.
Nikiwa nimeukunja uso kwa ghadhabu nikafika mapokezi. Yule dada usingizi ulikuwa umekatika!! Tukatazamana!!
Yeye anaogopa na mimi naogopa!!!
Maskini yule dada bila kujua kwamba ameambiwa anipatie kinga. Akadhani yule mbongo amemaanisha ule mkoba. Akaniomba msamaha kwa kila namna kisha kwa ukarimu kabisa akanipatia ule mkoba. Ulikuwa mzito kiasi. Nilipotaka kuondoka yule dada aliyekuwa amejikita katika kutafuta anachojua yeye, aliniita, nikageuka na kumshangaa kidogo.
“Unatakiwa kuweka sahihi.” Alinielezea kwa ukarimu.
Nikaona kama huyu binti ana nia mbaya na mimi. Nikabaki wima najiuliza iwapo niende mbele ama nirudi. Tukatazamana kwa sekunde kadhaa. Nikaona isiwe tabu. Nikarejea nikachukua kalamu niweze kuweka sahihi. Mara nikasikia fujo za mlango kufunguliwa.
Nikaomba Mungu usiwe mlango wa yule jamaa mbongo. Kisha nikasikia hatua kubwa kubwa zikitambaa.
“How long does it take to…to…..hell..” (Inachukua muda gani ku…ku…. ). Ilisikika sauti yenye kitetemeshi cha hasira. Alikuwa yule mbongo.
Sasa badala ya kuweka sahihi nikabaki kulishikashika tu lile daftari na kalamu. Mkojo ukatoka safari yangu ya mbali na sasa ulikuwa unahitaji kutoka. Nikabana miguu yangu!! Mkoba mkononi.
Ninafumaniwa Isabela mimi!!
Nikataka nikimbie!! Miguu ikawa mizito. Sikuwahi kufanya kitendo cha wizi hivyo lazima hali kama hii ingenitokea. UTATA.
ITAENDELEA!!!!

About Author

Advertisement

Post a Comment Blogger

Toa Maoni Yako Kuhusu habari Hii

Note: Only a member of this blog may post a comment.

 
Top